Ushairi
Shairi ni utungo wa kisanaa unaotumia lugha teule na Mpangilio maalumu wa maneno ili ujumbe unaokusudiwa uwasilishwe.
Sifa za Ushairi
Shairi huwa na umbo mahsusi
Hutumia lugha ya mkato
Huwa na beti,Mizani,Mishororo na vina
Hukiuka kanuni za kisarufi
Hutumia lugha teule yenye kuibua hisia nzito
Hutumia tamathali mbalimbali za usemi
Istilahi za kishairi
Hizi ni istilahi ambazo mwanafunzi wa ushairi anapaswa kutumia anapochambua mashairi.
Mshororo – ni msitari mmoja wa kifungu cha meneno.
Mizani – ni idadi ya silabi au vitamkwa katika kila mshororo.
Vina – ni silabi za mwisho katika kila kipande cha mshororo.
Ubeti – ni kifungu cha mishororo kadhaa katika shairi.
Vipande – ni visehemu katika mshororo vilivyogawanywa kituo (,).
Ukwapi – kipande cha kwanza cha mshororo.
Utao – kipande cha pili cha mshororo.
Mwandamizi – kipande cha tatu katika mshororo.
Ukingo – kipande cha nne katika mshororo.
Mwanzo – mshororo wa kwanza katika ubeti.
Mloto-mshororo wa pili katika ubeti.
Mleo – mshororo wa tatu katika ubeti.
Kimalizio/Kiishio – mshororo wa mwisho katika ubeti.
Kibwagizo- mshororo unaorudiwarudiwa katika kila ubeti.
Mashata-mshororo usiokamilika.
Kategoria za mashairi
Mashairi yamegawika katika makundi mawili makuu
Mashairi huru- haya ni mashairi yasiyozingatia kanuni za utunzi wa mashairi.
Mashairi ya arudhi- haya ni mashairi yanayozingatia kanuni.
Aina na bahari za mashairi
Aghalabu mashairi ya arudhi huainishwa kwa kuzingatia vigezo mbalimbali vya umbo kama vifuatavyo:
Idadi ya mishororo
Mpangilio wa maneno katika mishororo au beti
Idadi ya vipande vya mishororo
Mtiririko wa vina
urari wa mizani
Idadi ya mishororo
Zifuatazo ni aina za mashairi kwa kuzingatia kigezo cha idadi ja mishororo katika kila ubeti:
Aina Mishororo
Tathmina 1
Tathnia 2
Tathlitha 3
Tarbia 4
Takhmisa 5
Tasdisa 6
Usaba 7
Ukumi 10
Kigezo cha mtiririko wa Vina
Kigezo hiki huzalisha bahari tatu za mashairi ambazo ni:
Mtiririko -Hili ni shairi ambalo vina vyake vya kati na vya mwisho vinatiririka na havibadiliki kutoka ubeti wa kwanza hadi wa mwisho.
Ukara-_ Hili ni shairi ambalo vina vya kipande kimoja havibadiliki kutoka ubeti mmoja hadi mwingine,lakini vina vya kipande kingine hubadilika
Ukaraguni – shairi ambalo vina vyake vya kati na vya mwisho havitiririki, yaani hubadilika kutoka ubeti mmoja hadi mwingine.
Kigezo cha urari wa mizani
Kikai – Ni shairi ambalo lina mizani michache katika kipande kimoja cha mishororo kuliko kipande kile kingine, yaani hakuna urari wa mizani katika kila mshororo wa ubeti. Kwa hivyo, kipande kimoja huwa kifupi kuliko kingine, kwa mfano (5,8). Msuko-Ni shairi ambalo kibwagizo au mshororo wa mwisho ni mfupi kuliko mishororo mingine. Aghalabu huwa kina kipande kimoja tu kikilinganishwa na mishororo mingine yenye vipande viwili au vitatu, kwa mfano (8,8) (8,8) (8,8) (8).
Kigezo cha idadi ya vipande vya mishororo
Utenzi – shairi lenye kipande kimoja katika kila mshororo, aghalabu huwa na beti nyingi sana. Mizani huwa ni chini ya 12 katika kila mshororo.
Mathnawi – ni shairi la vipande viwili (ukwapi na utao) katika kila mshororo.
Ukawafi-ni shairi la vipande vitatu (ukwapi, utao na mwandamizi) katika kila mshororo.
Mavue – shairi la vipande vinne (ukwapi, utao, mwandamizi na ukingo) katika kila mshororo.
Kigezo cha mpangilio wa maneno katika mishororo au beti
Mkufu/Pindu/Nyoka – Hili ni shairi ambalo neno au kifungu cha maneno katika ubeti mmoja hutumiwa katika ubeti unaofuatia. Aghalabu, huwa ni kifungu au neno mwishoni mwa ubeti unaotangulia ndilo hutumiwa kutanguliza ubeti unaofuatia. Pia huweza kujitokeza popote kwenye ubeti.